Salamu – Aprili, 2020

Ni nawasalimu wapendwa woote katikajina la Bwana Yesu Kristo. Tunamshukuru sana Mungu ambaye ametupa mwezi huuwa nne. Naamini unajua kabisa kuwa kupewa mwezi mwingine ni neema kubwa mno.

Hasa katika kipindi hiki ambacho dunia inapitia janga kubwa la tauni ya corona. Na hapa nchini imefika na tayari watu wengi wameambukizwa na wengine wamefariki na serekali imetoa utaratibu wa nini kila mtu afanye ikiwemo kunawa kutokukaakwenye mikusanyiko na hata vyuo na shule zote kufungwa.

Ni kipindi kigumu mnoo, nchi zingine wamefungiwa watu ndani kwa kupewa amri ya kutokutoka nje. Tunashukuru serekali yetu imeweka utaratibu wa kila mtu afanye kazi na pia imeruhusu ibada. Hili ni jambo la kumshukuru Mungu sana.

Somo hili ambalo tunalipata hapa. Linaweza kukusaidia sana katika kilindi hiki. Ngoja nikupe taarifa fupi ya mwezi uliopita. Mwezi uliopita tulikua na semina Bethlehemu na Mbalizi Bethani Kkkt. Semina hii tulianza nayo mwishoni mwa mwezi wa pili na tukaendelea nayo mpaka tarehe tano mwezi wa nne.

Ninapokuletea salamu hizi nipo jijini Mbeya kwasababu ratiba yetu ya mwezi huu ilikua tuwe Dodoma na Manyoni. Kutokana na mambo yaliyo nje ya uwezo wetu semina hizi tumeziahirisha.

Hiyo ndiyo taarifa fupi ya huduma mwezi uliopita. Ebu tusogee mbele kidogo katika salamu za mwezi huu. Kumbuka tuna salamu zenye kichwa.

MAMBO MUHIMU UNAYOTAKIWA UYAFANYE ILI UPATE WOKOVU (ENEO LA KUOKOLEWA KATIKA KIPINDI CHA MAJANGA ULIMWENGUNI)

Tuangalie jambo la tano

JAMBO LA TANO JIFUNZE KUFANYA TOBA BILA KUANGALIA UKAMILIFU WOWOTE

Sikiliza, Unapomwendea Mungu katika kipindi hiki cha kumwomba kwa ajili ya wokovu wa tauni au nzinge nk iliyopelekwa na Mungu, unatakiwa wewe kama kuhani uhakikishe moyoni mwako unaondoa ile hali ya kujiona uko msafi.

Angalia mistari hii uone. “Maana kila kuhani mkuu aliyetwaliwa katika wanadamu amewekwa kwa ajili ya wanadamu katika mambo yamhusuyo Mungu, ili atoe matoleo na dhabihu kwa ajili ya dhambi; awezaye kuwachukulia kwa upole wao wasiojua na wenye kupotea, kwa kuwa yeye mwenyewe yu katika hali ya udhaifu; na kwa sababu hiyo imempasa, kama kwa ajili ya watu, vivyo hivyo kwa ajili ya nafsi yake mwenyewe, kutoa dhabihu kwa ajili ya dhambi.Na hapana mtu ajitwaliaye mwenyewe heshima hii, ila yeye aitwaye na Mungu, kama vile Haruni. Vivyo hivyo Kristo naye hakujitukuza nafsi yake kufanywa kuhani mkuu, lakini yeye aliyemwambia, Ndiwe mwanangu, Mimi leo nimekuzaa. kama asemavyo mahali pengine, Ndiwe kuhani milele Kwa mfano wa Melkizedeki. Yeye, siku hizo za mwili wake, alimtolea yule, awezaye kumwokoa na kumtoa katika mauti, maombi na dua pamoja na kulia sana na machozi, akasikilizwa kwa jinsi alivyokuwa mcha Mungu;” (Waebrania 5:1-7)

Ukiitazama hiyo mistari utaona tunafundishwa hapo kuwa, kuhani yeye mwenyewe anapomwendea Mungu inatakiwa atubie kwanza uovu wake. Kama anatakiwa atubue uovu wake maana yake anao.

Unaposoma maandiko ni kuhani wetu mkuu Bwana Yesu Kristo peke yake ndiye ambaye hakuwa na hatakuwa na dhambi.(Hakufanya ingawa alichukua dhambi za ulimwengu)

Katika kipindi cha kuutafuta uso wa Mungu makuhani lazima tujihadhari na mtazamo wa moyoni wa kujihesabia haki kama hao wengine woote tuwaonao wakikumbwa na hili tatizo kama ni wadhambi mnoooo kuliko sisi. MWENYE MASIKIO NA ASIKIE!!!!!

Ondoa moyoni mwako wazo kuwa Mungu atakusikia kwa sababu wewe ni mwenye matendo mema kuliko wengine, hapana. Mungu atakusikia kwa sababu kuu moja tu: umeona kosa lako wewe na hao wengine woote na umeamua kuliungama na kujutia. Ndiyo maana ya unyenyekevu.

Ngoja nikupe mfano huu uone hiki ninachotaka nikutazamishe Angalia Danieli alivyomwendea Mungu katika kipindi ambacho aliwakasirikia wa wa Israeli

“Katika mwaka wa kwanza wa Dario, mwana wa Ahasuero, wa uzao wa Wamedi, aliyetawazwa kuwa mfalme juu ya milki ya Wakaldayo; katika mwaka wa kwanza wa kumiliki kwake, mimi Danieli, kwa kuvisoma vitabu, nalifahamu hesabu ya miaka, ambayo neno la BWANA lilimjia Yeremia nabii, ya kuutimiza ukiwa wa Yerusalemu, yaani, miaka sabini. Nikamwelekezea Bwana Mungu uso wangu, ili kutaka kwa maombi, na dua, pamoja na kufunga, na kuvaa nguo za magunia na majivu. Nikamwomba BWANA, Mungu wangu, nikaungama, nikasema, Ee Bwana, Mungu mkuu, mwenye kutisha, ashikaye maagano na rehema kwao wampendao, na kuzishika amri zake; tumefanya dhambi, tumefanya ukaidi, tumetenda maovu, tumeasi, naam, hata kwa kuyaacha maagizo yako na hukumu zako; wala hatukuwasikiliza watumishi wako, manabii, ambao kwa jina lako walisema na wafalme wetu, na wakuu wetu, na baba zetu, na watu wote wa nchi. Ee Bwana, haki ina wewe, lakini kwetu sisi kuna haya ya uso, kama hivi leo; kwa watu wa Yuda, na kwa wenyeji wa Yerusalemu, na kwa Israeli wote, walio karibu na hao walio mbali, katika nchi zote ulikowafukuza, kwa sababu ya makosa yao waliyokukosa. Ee Bwana, kwetu sisi kuna haya ya uso, kwa wafalme wetu, na wakuu wetu, na baba zetu, kwa sababu tumekutenda dhambi. Rehema na msamaha ni kwa Bwana Mungu wetu, ingawa tumemwasi; wala hatukuitii sauti ya BWANA, Mungu wetu, kwa kwenda katika sheria zake, alizoziweka mbele yetu kwa kinywa cha watumishi wake, manabii. Naam, Israeli wote wameihalifu sheria yako, kwa kugeuka upande, wasiisikilize sauti yako; basi kwa hiyo laana imemwagwa juu yetu, na uapo ule ulioandikwa katika sheria ya Musa, mtumishi wa Mungu; kwa sababu tumemtenda dhambi.” (Danieli 9:1-11)

Ukiisoma hiyo mistari kumi na moja utagundua Danieli alikuwa anautafuta uso wa Mungu ili Mungu awaondolee adhabu ambayo aliwapelekea kwa sababu walimkasirisha. Aliwapeleka utumwani.

Danieli anaposimama ili azungumze na Mungu, kwanza alijua kabisa kuwa kisa cha tatizo wanalopitia ni dhambi, na alijua kabisa kuwa wanapitia adhabu kali sana.

Alipokuwa anaziungama dhambi mbele za Mungu, Danieli hakujihesabia haki kabisaa.

Sikiliza anasema hivi: “Nikamwomba BWANA, Mungu wangu, nikaungama, nikasema, Ee Bwana, Mungu mkuu, mwenye kutisha, ashikaye maagano na rehema kwao wampendao, na kuzishika amri zake; tumefanya dhambi, tumefanya ukaidi, tumetenda maovu, tumeasi, naam, hata kwa kuyaacha maagizo yako na hukumu zako;wala hatukuwasikiliza watumishi wako, manabii,”

Sikiliza kwa makini hayo maombi. Hasemi Wamefanya dhambi, hawajaisikiliza sauti ya watumishi wako, nk. Anasema TUMEFANYA DHAMBI!!!!

Angalia kitu cha ajabu hapo, Daniel ni mtumishi wa Mungu kabisaa yeye ni nabii.angalia anasema hatukuwasikiliza watumishi wako. Anapotubu na kuungama anajihesabu yeye na hao wana wa Israeli ni wakosaji, ingawa kwa kweli utaona yeye huenda hakuifanya hiyo dhambi.

Sikiliza Bwana Yesu Kristo kama kuhani mkuu, aliichukua dhambi ya ulimwengu, unajua maana ya kuuichukua dhambi ya ulimwengu? Maana yake ni hii yeye alijitwisha hiyo dhambi kama ni yeye amefanya, ndiyo maana ya kuchukua dhambi ya ulimwengu.

Kwa maana nzuri maombi yake alisema vivyo hivyo kama alivyosema Danieli. Tumekutenda dhambi, nk!!! Hakuwa na mtazamo kama huu wa kusema wamefanya dhambi …..

Ngoja nikuambie kitu; unapoiombea nchi yako ya Tanzania ili Mungu aiokoe katika majanga ya namna Hii, Unajua ni rahisi sana mpendwa ukiwa humu ndani ya nchi hii ukaona kama hao watu wa nchi za Ulaya, China, Amerika, Uarabuni n.k kama ni watu waovu kweli.

Ni rahisi kuona aisee Wachina bwana hawana Mungu wale ndiyo maana Mungu anawachapa kwa tauni hii ya Corona, nirahisi kufikiri wazungu bwana wako tofauti na sisi Waafrika, wamemuacha Mungu, ndiyo maana ameamua kuwachapa. n.k.

Sikiliza mpendwa ukitaka leo hii kuwa kuhani wa ulimwengu yaani ukasimama mahali palipoharibika ulimwenguni jifunze kuomba maombi ya mfumo wa kutokuwaona hao ni waovu.

Ukisikia vita sehemu nchi furani usifikiri wa Tanzania ni watu watakatifu kuliko hao wa taifa hilo. Au ukisikia nzinge na tauni inazipiga nchi furani usifikiri sisi huku ni bora kuliko hao. Unapokwenda kuomba ulinzi kwa Mungu tubu mpendwa bila kujiona wewe ni bora.

Mimi naamini sisi Watanzania tutaokolewa tu kwa maombi ya toba na unyenyekevu. Si kwa sababu eti tuna Mungu.

Ngoja nikuulize swali wewe usemaye unajua hao wazungu walimwacha Mungu nk. Hivi kweli sisi Waafrika tuna Mungu?  Hivi sisi Waafrika hatuna maovu? Wewe angalia namna tunavyoabudu miungu, angalia uzinzi, angalia uchawi, angalia namna wanaume wasivyowatunza wake zao na watoto.

Mungu anasema  hivi “Lakini mtu ye yote asiyewatunza walio wake, yaani, wale wa nyumbani mwake hasa, ameikana Imani, tena ni mbaya kuliko mtu asiyeamini.”(1 Timotheo 5:8)

Maana yake Mkristo wa sifa hiyo hana tofauti na mpagani aliyesema hakuna Mungu.

Angalia nchi hii ilivyo na damu za watu wengi tu katika ardhi. Watu wengi hutoa mimba na kuua katika nchi hii nakuambia. Nchi hii ndiyo unasikia watu wanaua wanadamu wenzao wenye ulemavu wa ngozi ili tu wapate mali au ukuu, n.k.

Nchi hii ina watu wengi mnooo wanaoamini ushirikina, n.k mtu haolewi mpaka akaloge, akiolewa analoga ili mume akae naye.

Nenda kanisani uone dhambi zipo nje nje, si watumishi na waaminio kila siku unaona na kusikia wameanguka na hata kuwa waongo angalia watu wengi mnoo wamejeruhiwa na kuumizwa mno na sisi watumishi katika nchi hii n.k.

Angalia dhambi ya uongo na udanganyifu nk. Mimi nimejaliwa kutembea nchini humo, aisee nchi hii ina makahaba wengi mnoo na wengine wako makanisani kabisaa.

Angalia humo makanisani namna tupatavyo viongozi, wewe angalia namna nchi hii tunavyopata viongozi nk. Wengi hutoa rushwa nk.

Angalia kanisani namna tunavyoiba fedha na sadaka ya Mungu nk. Umewahi ona mradi wa kanisa unaenda?

Angalia wivu na husuda na kudhulumu wajane na mayatima nchini humu tulivyo.

Angalia dhambi ya uvivu na kutolipa kodi sijakosea nasema kodi jinsi tulivyo.

Angalia namna tunavyoiba hiyo kodi ya serikali jinsi tulivyo. Angalia dhambi ya ulevi jinsi ilivyo nchini mwetu.

Kwa haya tu ninayokuambia unaweza ukaniambia sisi tupo salama kuliko hao wanaokufa huko na Corona? Na nchi zao kuliwa na nzinge nk?

Sikilizeni makuhani hebu tuondoe hayo mawazo ya kitoto kuwa sisi tuna haki kama taifa kuliko mataifa mengine.

Wengine wanasema unajua sisi Waafrika mafua hayatatudhuru. Sikia ni tauni. Kama tusipomwomba Mungu kwa unyenyekevu mafua tunayofikiri tutayamudu; yatatumudu nawaambia.

Katika kipindi kama hicho tusijiangalie tulivyo tunahitaji TUMRUDIE MUNGU KWA KILIO BILA KUJIHESABIA HAKI. TUKUBALI KUWA TUMEMKOSEA MUNGU NA ANA HAKI KABISAA YA KUTURUDI. KINACHOTAKIWA TUKIFANYE TUSIJIONE NI WENYE HAKI.

Hatuna haki tuungane makuhani tumwambie BWANA TUMEKUFANYIA DHAMBI.

Danieli naamini hakufanya hayo maovu lakini alilijua hili ninalokuambia alisema tumekufanyia dhambi sisi na Israeli woote!!

Ukiwa ni mtu wa tabia hii Mungu nirahisi kukuokoa wewe na nyumba yako.Mungu

alimsikia. Danieli na makuhani wengine, fahamu hata wewe na mimi atatusikia tu. Hebu chukua hii na uanze kuliweka kwenye matendo.

Tuonane katika katika salamu za mwezi ujao.

Ukihitaji masomo yetu unaweza kuyapata kwa njia hizi zifuatazo:-

  1. App yetu ya huduma yenye jina  “MWAKATWILA (HUSONEMU)” utaipata Play Store ambapo kuna masomo mengi sana hapo.
  2. Tovuti yetu ya www.mwakatwila.org
  3. YouTube – Mwakatwila au HUDUMA YA SOMA NENO LA MUNGU (HUSONEMU).
  4. Facebook ingia katika hiyo tovuti (website) yetu utaona alama ya Facebook (f) “like” na utapata maelezo ya kujiunga au ingia Facebook halafu andika “SOMA NENO LA MUNGU”
  5. Instagram ingia Instagram app halafu andika “Steven Mwakatwila”
  6. DVDs au CDs
  7. VITABU. Wasiliana na mhudumu ofisini kwa namba +255 763 109 733, ili kupata VITABU, DVD & CD.
  8. Kwa njia ya REDIO:- Utapata mafundisho yetu kwa redio zifuatazo:-
    • Rungwe FM 102.5 Kila siku ya Jumapili  saa tatu mpaka saa nne usiku.
    • Baraka FM 107.7 Kila siku ya Jumanne saa kumi na mbili jioni mpaka saa moja usiku.
    • Bomba FM 104.1 Kila siku ya Ijumaa saa tatu usiku mpaka saa nne usiku.
  9. Unaweza kutupata kwenye ONLINE RADIO yetu:-  radio.mwakatwila.org

Kwa Mawasiliano zaidi Utatupata kwa namba hizi:-

+255 754 849 924 au +255 756 715 222

Wako

Mwl Mr & Mrs Steven Mwakatwila.