Salamu – Juni, 2024

Bwana Yesu Kristo asifiwe. Ndugu zangu leo hii ninakuletea salamu za mwezi wa sita.  Tunamshukuru sana kwa maombi yako. Mwezi wa tano tumekua na semina nyingi sana. Tulianza semina kwa hema ambalo Mungu ametupa na tunatumia kufundishia nchini na nje ya nchi.

Tulianzia semina hizo jijini Mbeya. Tukaenda Kigoma mjini,Tukaenda Mpanda,Tukaenda Sumbawanga tukimaliza tunaenda Tunduma mkoa wa Songwe. Tumekua na semina nzuri sana sana. Ukitaka kufuatilia masomo hayo nenda kwenye youtube Mwakatwila TV. karibu sana.

Pia usisite kufuatilia mawasiliano nasi unapofikia mwisho kwenye salamu zetu za mwezi.

Leo hii tusogee mbele kidogo….karibu tuzipokee salamu hizi.

USIKIMBILIE KUTAFUTA HUDUMA KISA UNA KARAMA ZA ROHO

Moja ya jambo muhimu la kulijua ni hili la mtu aliyepewa karama za roho usijitafutie ofisi ya kihuduma kisa kwadababu umepewa karama za roho kama karama za kuponya,karama za unabii,karama za matendo ya miujiza nk.

Watu wengi hapa ndipo wamebanwa..Watu wengi kwa kutokujua kuhusu habari za karama za roho wamejikuta wakifanya huduma ya Nabii kisa ni kwa sababu wanapokea unabii.

Wengine leo hii wameanzisha huduma za kuchunga wakati wana karama za kuponya au karama za matendo ya miujiza. Ili kanisa likue na likamilishwe ni lazima kila mtu akae kwenye eneo lake. Yaani ofisi za kihuduma zikae mahali pake na wenye karama za roho akae mahali pake.

Unapokua umepewa karama za roho na wewe ukaanza kujitafutia kuchunga nk fahamu watu wote waliochini yako watapotea tu. Unajua ni kwanini? Angalia mistari hii tena “Naye alitoa wengine kuwa mitume, na wengine kuwa manabii; na wengine kuwa wainjilisti na wengine kuwa wachungaji na waalimu; kwa kusudi la kuwakamilisha watakatifu, hata kazi ya huduma itendeke, hata mwili wa Kristo ujengwe;hata na sisi sote tutakapoufikia umoja wa imani na kumfahamu sana Mwana wa Mungu, hata kuwa mtu mkamilifu, hata kufika kwenye cheo cha kimo cha utimilifu wa Kristo;”(Waefeso 4:11-13)

Kiukweli watu walioitwa kwenye hizo ofisi tano ndiyo waliyopewa upako wa kuwakamilisha hao watakatifu.

Sasa sikia wewe haujapewa upako huo wewe umepewa upka wa karama za roho..kwako ni ngumu kuwa kamilisha hawa watakatifu. Ngoja nikupe mfano fuatilia watu waliochini ya mtu mwenye karama za roho hawezi kuwachunga hao watu. Kazi za mchungaji ni hizi. “BWANA ndiye mchungaji wangu, Sitapungukiwa na kitu.Katika malisho ya majani mabichi hunilaza, Kando ya maji ya utulivu huniongoza.Hunihuisha nafsi yangu; na kuniongoza Katika njia za haki kwa ajili ya jina lake.” (Zabibu 23:1-3).

Zitazame hapo sifa za mchungaji. kanisa likikosa mchungaji halikui kabisaa, halikui kwasababu chakula cha kiroho kinaletwa na wachungaji ili kondoo wale na kunywa..mtu mwenye karama za roho yeye anaponya tu..hawezi kuchunga nakwambia.

Ukilitazama kanisa lilivyo utagundua hili ninalo kuambia, ukikaa chini ya Nabii ambaye ana leta unabii watu waliochini yake hawachungwi,hawafundishwi,hawana neno la Mungu lililo ndani ya Biblia. Na kwa kuwa unabii unapimwa kwenye neno lililo ndani ya Biblia utawaona watu walio chini ya manabii wanakosa neno la Mungu la kuwaongoza wengi hupotea.

Ukikaa chini ya watu wanaoongozwa kwa kufuata miujiza tu utawaona watu hao leo hii hupenda miujiza kuliko kumpenda Bwana Yesu Kristo. Wakikosa miujiza tu hupoteza imani yao kwa Bwana Yesu Kristo. Sikia Mungu hataki sisi tuishi kwa miujiza, sisi tunaishi kwa imani na imani inaletwa na neno la Bwana Yesu Kristo. Sasa ukikaa chini ya mtu wa miujiza fahamu miujiza si ya kudumu, ina mwisho.

Ngoja nikupe mfano, ukikaa chini ya mtu mwenye matendo ya miujiza leo atawapa chakula kimiujiza, lakini ujue kuwa kesho muujiza huo utakoma. Angalia Mungu anapoleta muujiza wa kukutunza fahamu ipo siku muujiza huo utakufa. wana Waisraeli waliletewa mana..siku moja mana ilikoma, Eliya alitunzwa kimiujiza wa kuletewa na kunguru, na huko kwa mwanamke mjane.

Siku moja kijito kilikatika,kunguru aliacha kumletea Eliya chakula, na kuna siku pipa la unga lilikoma. Sikia, ukiwa ni mtu uliyepewa karama za matendo ya kimiujiza ujue kuwa wewe si mchungaji wala si mwalimu. Usijianzishe huduma za kuchunga au kufundisha wakati haujaitwa uwe umeitwa katika huduma hizo utawapoteza watu nakwambia.

Watu wengi wenye karama hizi za roho za kuponya na matendo ya miujiza wanapofuatwa na watu wengi hupata wazo la kuwakusanya hao watu na kuanza kuwamiliki ili wawe chini yao.

Sikia usipokua na hekima utakutana siku moja na Bwana Yesu Kristo aliyewaambia watumishi wale ambao walitoa unabii kwa jina la Bwana na walifanya miujiza kwa jina la Bwana lakini alisema hawajui.

Unajua ni kwa nini aliwaambia hawajui? Ni kwasababu hawakutenda mapenzi ya Mungu. Sikia ni mapenzi ya Mungu kila mtu amtumikie Mungu kwenye ofisi aliyompa na aitumie karama za roho alizompa mahali alipotaka azitende.

Ngoja nikuulize swali kunashida gani leo ukiwa na karama za roho na ukawa na mchungaji wako na mwalimu wako? Hebu tuache kutafuta utukufu na sifa.

Ukiwa mnyenyekevu huwezi kupata shida leo hii kumheshimu mtumishi wa Mungu kisa eti wewe unakarama za roho.

Naamini umeelewa. Tuonane tena katika kona hii ya salamu za mwezi.

Ukihitaji masomo yetu unaweza kuyapata kwa njia hizi zifuatazo:-

  1. App yetu ya huduma yenye jina “MWAKATWILA (HUSONEMU)” utaipata Play Store ambapo kuna masomo mengi sana hapo.
  2. Tovuti yetu ya www. mwakatwila. org
  3. YouTube – Mwakatwila au HUDUMA YA SOMA NENO LA MUNGU (HUSONEMU).
  4. Facebook ingia katika hiyo tovuti (website) yetu utaona alama ya Facebook (f) “like” na utapata maelezo ya kujiunga au ingia Facebook halafu andika “SOMA NENO LA MUNGU”
  5. Instagram ingia Instagram app halafu andika “Steven Mwakatwila”
  6. DVDs au CDs
  7. VITABU. Wasiliana na mhudumu ofisini kwa namba +255 763 109 733, ili kupata VITABU, DVD & CD.
  8. Kwa njia ya REDIO: – Utapata mafundisho yetu kwa redio zifuatazo:-
  • Rungwe FM 102. 5 Kila siku ya Jumapili saa tatu mpaka saa nne usiku.
  • Baraka FM 107. 7 Kila siku ya Jumanne saa kumi na mbili jioni mpaka saa moja usiku.
  • Bomba FM 104. 1 Kila siku ya Ijumaa saa tatu usiku mpaka saa nne usiku.

Unaweza kutupata kwenye ONLINE RADIO yetu:- radio.mwakatwila.org

Kwa Mawasiliano zaidi Utatupata kwa namba hizi:- +255 754 849 924 au +255 756 715 222

Wako: Mwl Mr & Mrs Steven Mwakatwila.